OBAMA , ZUMA ANA KWA ANA

Rais wa Marekani Barack Obama, amesema uvumilivu na ujasiri wa Nelson Mandela ni mfano mwema kwa dunia na upendo wa dhati wa rais huyo wa zamani wa taifa la Afrika Kusini inaonyesha ni kwa namna gani alivyo na utu wa kibinadamu.
Bwana Obama ameongeza kuwa Mandela, alionyesha ukweli na ukakamavu ambao una maana kubwa katika utu wa kibinadamu ambao uliondoa tabaka la ubaguzi, udini na utaifa.
Rais huyo wa marekani ameyazungumza hayo mjini Pretoria baada ya mazungumzo na rais wa sasa wa Afrika kusini, Jacob Zuma.
Ziara hiyo ya bwana Obama ina lengo la kuongeza mauhusiano ya kibiashara lakini imetekwa na hisia za ugonjwa wa bwana Mandela ambaye amelazwa hospitalini kwa muda wiki tatu sasa kutokana na maradhi ya mapafu yanayosumbua mfumo wake wa kupumulia.
Katika kikao hicho wawili hao walizungumza na vyombo vya habari kuhusu ushirikiano wa mataifa yao kibiashara mbali na kutafuta suluhu ya kudumu katika mataifa yaliokumbwa na ghasia mashariki ya kati.
Ikulu ya White House imesema kuwa Obama pia atakutana na familia ya Mandela anayeugua maambukizi ya mapafu ili kuifariji.
Awali Rais Obama, aliye ziarani barani afrika alitoa shukran za dhati kwa uongozi ulioonyeshwa na Mandela.
Wakati wa ziara hiyo Obama pia atakutana na wanafunzi huko Soweto kabla ya kuelekea katika jela la Robben Island ambayo Mandela alihudumia kifungo chake cha miaka 27 wakati wa utawala wa ubaguzi wa rangi.


Share: