TUME YAUNDWA KUCHUNGUZA MLIPUKO WA BOMU-ARUSHA

Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Mwema ameunda timu ya kuongeza nguvu ya uchunguzi itakayoongozwa na makamishna wawili ambao ni Paul Chagonja kutoka idara ya operesheni na Isaya Mngulu kutoka ofisi ya upelelezi makao makuu.

IGP Mwema alisema baada ya tukio hilo, jeshi hilo lilituma makamishna wawili kutoka makao makuu kwa ajili ya kuongeza nguvu ya uchunguzi wa tukio hilo na kwamba wameshaanza kukusanya taarifa mbalimbali zitakazoweza kusaidia kuwabaini watu waliohusika.

Alisema wameunganisha nguvu na vyombo vingine vya ulinzi na watawasaka wahalifu hao pamoja na walio nyuma yao kwa kile alichoeleza tukio hilo linaashiria kushamiri kwa matendo ya kigaidi nchini.

Akizungumzia tuhuma zinazotolewa na wananchi juu ya Jeshi la Polisi kuwajeruhi watu kwa risasi za moto, IGP Mwema alisema kila taarifa inafanyiwa kazi kwa umakini na kwamba baada ya uchunguzi watatoa taarifa kamili kwa umma juu ya kilichotokea jijini Arusha.

Aliwaomba wananchi wenye taarifa za kuweza kumtambua aliyerusha bomu pamoja na watu walio nyuma yake wajitokeze au wamtumie ujumbe kupitia simu yake ya mkononi namba 0754 78 55 57 na kwamba uhusika wao utafanywa kuwa siri.

IGP Mwema pia alisema watachunguza kauli ya Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) bara, Mwigulu Nchemba aliyowaambia wakazi wa Kimandolu kuwa wasipoichagua CCM katika uchaguzi wa madiwani wa Jiji la Arusha ulioahirishwa jana, watakufa.

Mwema alisema watachunguza kauli hiyo baada ya kuulizwa swali la hatua zilichochukuliwa kabla na baada ya mlipuko huo dhidi ya kauli ya Nchemba.

Juzi katika mkutano wa kufunga kampeni za udiwani kwa CHADEMA uliofanyika kwenye viwanja vya Soweto, kitu kinachodhaniwa ni bomu kilipuka na kuua watu watatu na wengine kujeruhiwa.


Share: