AMBULACE ILIYOMBEBA MANDELA YAHARIBIKA NJIANI KWENDA HOSPITALI

Gari la waGonJwa lililokuwa likimsafirisha hospitalini rais wa zamani wa Afrika Kusini Nelson Mandela wiki mbili zilizopita, liliharibika likiwa njiani kwenda hospitalini.

Msemaji wa rais wa Afrika Kusini Mac Maharaj, amethibitisha kuwa gari hilo lilikumba na matatizo na kuwa ilibidi rais huyo wa zamani kuhamishwa hadi gari lingine.
Hata hivyo Bwana Maharaj, amesema tukio hilo halikuwa na tishio lolote kwa afya ya Bwana Mandela, kwa sababu alikuwa na madaktari wa kutosha.
Shirika la habari la Marekani CBS limenukuu vyanzo kadhaa vikidai kuwa Mandela alisalia katika eneo hilo kwa zaidi ya dakika arubaini kabla ya usaidizi kufika.
Shirika hilo la CBS limesema kuwa wakati Bwana Mandela alipokuwa akihamishwa hadi gari lingine viwango vya joto vilikuwa chini sana.
Mandela, mwenye umri wa miaka 94, alikuwa akisafirishwa kutoka hospitali moja mjini Johannesburg hadi Pretoria, wakati wa tukio hilo lililotokea tarehe nane Juni mwaka huu.
Mandela alilazwa hospitalini huku hali yake ikiwa mbaya kutokana na maambukizi ya mapafu ya mara kwa mara na tangu wakati huo amekuwa katika chumba cha wagonjwa mahututi.
Hii ni mara ya tatu kwa Bwana Mandela kulazwa hospitalini mwaka huu.


Share: