HIVI NDIVYO PANYA WANAVYOTUMIKA KUGUNDUA MABOMU ARDHINI

Shirika moja lisilo la kiserikali la Ubelgiji APOPO limeanza kuwafundisha panya namna ya kutambua mabomu yaliyofukiwa ardhini. Panya hao ambao ni wakubwa kuliko panya wa kawaida wanafanyiwa majaribio Morogoro Tanzania .Inaaminika wanauwezo mkubwa wa kunusa kuliko mbwa. Hii inatokana na kuwa pua zao zipo karibu na ardhi,hali ambayo inawasaidia katika kazi yao ya utambuzi wa mabomu.


Panya wanafundishwa jinsi ya kunusa wakiwa wadogo, kwa kuwekewa vitu vyenye madini ya milipuko.Tangu mwaka 2000, APOPO imekuwa ikiwafunza panya kwenye chuo cha Sokoine,Morogoro. Mwaka 2006 panya wa hao walianza zoezi la kutafuta mabomu ya ardhini huko Msumbiji. Kabla ya panya kuanza kazi ya kunusa wapi mabomu yalipo, lazima wafuzu mtihani kutimiza viwango vya kimataifa vya kutambua mabomu ardhini.


Panya hujifunza kufuata eneo fulani hatua kwa hatua. Waya au kamba hufungwa mwilini kutoka kwenye ufito. Wasimamizi wawili husimama kila upande wa ufito na kumruhusu panya kutembea toka mwanzo wa ufito hadi upande mwingine kwa kufuata jinsi waya au kamba alizo fungwa mwilini. Katika mafunzo ya awali panya hufunzwa kunusa kemikali aina ya TNT ndani ya chombo cha chuma


Baadaye kila panya hufanya mafunzo kwenye eneo ambalo kuna mabomu ya ardhini yaliyofukiwa na vifaa ambayo huzuia mlipuko. Ikiwa panya ameweza kunusa na kutambua yalipo madini asilia ya TNT huwa anasimama na kuanza kufukua sehemu hiyo ya ardhi iliyofukiwa bomu. Kuwafundisha panya kunachukua muda wa mwaka na inagharimu dola za Kimarekani $6,000 sawa na Euro 4,670



Wakati wa mafunzo panya hupewa zawadi kwa kufuzu vizuri kwa sauti maalumu ambayo inaashiria kufuzu kwake na kupewa kipande cha ndizi kama zawadi. Panya aliyefuzu vizuri huwa ana uwezo wa kuzunguka mita 400 za mraba kwa siku, wakati eneo kama hili litamchukua binadamu wiki mbili ili kuweza kugundua wapi kumefukiwa bomu



Kulinganishwa na mbwa, panya wanaweza kutumiwa na mtu yeyote kwani hawana tabia ya kutokuwa na mahusiano ya karibu na mtu aliyemfundisha kama walivyo mbwa. Panya anaweza kufanya kazi ya kufichua mabomu, hata kama aliyemfundisha hayupo na huwa wanafanya kazi vizuri kwa ufanisi na mtu yeyote. Hakuna shida kwa panya aliyefundishwa Tanzania, kwenda kufanya kazi Msumbiji, Angola,Thailand na Kambodia



Hadi kufukia sasa nchini Msumbiji, zaidi ya mita za mraba milioni 6,5 za ardhi zimeshachunguzwa na mabomu 2,000 yaliyotegwa ardhini yamepatikana na kuharibiwa, pia bado mabomu 1,000 kuteguliwa na bunduki na silaha nyingine ndogo 12,000 zilipatikana. Na mpaka sasa kuna makundi saba yenye watu 54 ambayo yanashughulika na kazi ya kutegua mabomu kwa kuwatumia panya


Share: